Monday, 24 March 2014

WAAMUZI WATAO AFRIKA KUCHEZESHA KOMBE LA DUNIA

Afrika itawakilishwa na waamuzi wa kati watatu kwenye fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika Brazil kwa mujibu wa orodha ya waamuzi 25 iliyotolewa na Shirikisho la Soka Kimataifa (FIFA. Kila mwamuzi ataongoza timu ya wasaidizi wawili na hivyo kufanya idadi ya waamuzi wasaidizi kutoka Afrika kuwa nane kati ya 50.
Fainali za Kombe la Dunia 2014 zitafanyika nchini Brazil kuanzia Juni 12 mpaka Julai 13 ikiwa ni mara ya pili kwa fainali hizo kufanyika kwenye nchi hiyo kigogo katika soka duniani. Mara ya kwanza fainali hizo zilifanyika Brazil mwaka 1950.
Waamuzi hao ni Doue Noumandiez kutoka Ivory Coast, Papa Gassama (Gambia) na Djamel Haimoudi (Algeria) ambao wataongoza timu ya waamuzi watatu kila mmoja kwenye fainali hizo, kwa mujibu wa utaratibu wa FIFA.
Doue atachezesha mechi za fainali hizo pamoja na waamuzi wasaidizi kutoka Burundi, Songuifolo Yeo na Jean Claude Birumushahu.
Gassama ataunda timu itakayowajumuisha waamuzi wasaidizi Evarist Menkouande kutoka Cameroon na Kabanda Felicien kutoka Rwanda, wakati Haimoudi ataongoza waamuzi wasaidizi Abdelhak Etchiali wa Algeria na Redouane Achik wa Morocco.
Mwamuzi wa akiba kutoka Afrika Kusini Daniel Bennett na Neant Alioum kutoka Cameroon wanakamilisha orodha hiyo ya waamuzi kutoka Afrika. Katika orodha hiyo pia wamo Djibril Camara (Senegal) na Marwa Range (Kenya).
Afrika imeendelea kushikilia idadi yake ya waamuzi watatu wa kati kwenye fainali hizo.
Kwa mujibu wa orodha ya FIFA waamuzi wengine ni Ravshan Irmatov kutoka Uzbekistan, Yuichi Nishimura (Japan), Nawaf Shukralla (Bahrain), Benjamin Williams (Australia), Joel Aguilar (El Salvador), Mark Geiger (Marekani), Marco Antonio Rodriguez (Mexico), Enrique Osses (Chile), Nestor Pitana (Argentina), Sandro Ricci (Brazil), Wilmar Roldan (Colombia), Carlos Vera (Ecuador), Peter O’Leary (New Zealand), Felix Brych (Ujerumani), Cuneyt Cakir (Uturuki), Jonas Eriksson (Sweden), Bjorn Kuipers (Uholanzi), Milorad Mazic (Serbia), Pedro Proenca (Ureno), Nicola Rizzoli (Italia), Carlos Velasco (Hispania) na Howard Webb (England).
Mbali na Afrika, bara la Ulaya litatoa waamuzi tisa, Shirikisho la Soka la Amerika ya Kusini (CONMEBOL) litatoa waamuzi watano, huku waamuzi wanne wakitoka Asia (AFC), watatu kutoka Shirikisho la Soka la vyama vya Amerika ya Kaskazini na Visiwa vya Carribea (CONCACAF) na mmoja kutoka Oceania.
Akizungumzia uteuzi wa waamuzi hao 25, Katibu Mkuu wa Fifa, Jerome Valcke alisema: “Waamuzi hao walichaguliwa kutokana na uwezo wao, uelewa wao wa mchezo wa soka, uwezo wa kuusoma mchezo na kuelewa timu zinazocheza zinatumia mbinu gani.”
Hata hivyo Valcke alisema kuna baadhi ya waamuzi na wasaidizi wao wanaweza kuachwa Juni 12 wakati watakapowapima kwa mara ya mwisho ili kujua kama wapo fiti kabla ya kuanza kwa mashindano.
Alisema: “Fifa ina utaratibu wa kuchagua waamuzi bora ambao wapo fiti kwa ajili ya kuchezesha Fainali za Kombe la Dunia. Huwa tunachagua waamuzi ambao wapo katika ubora wa juu kabla ya mashindano.”

< mwananchi>

No comments:

Post a Comment