Maiti ya Adrian Louis iliokotwa kando ya barabara kuu ya kwenda Lukuledi wilayani Masasi katika Mkoa wa Mtwara.
Haikuwa na jeraha lolote. Ndugu zake walipopata taarifa za msiba, waliuchukua mwili na kuusitiri harakaharaka.
Hawakuwa na wasiwasi wowote wa kutaka kujua chanzo
cha kifo cha ndugu yao kwani waliamini kuwa amefariki dunia kwa sababu
ya kuzidiwa na ulevi, kwa kuwa siku zote alikuwa mlevi kupindukia.
Kumbe, walikuwa wamekosea, kwani siku hiyo Louis hakuwa amelewa, bali
kifo chake kilisababishwa na majambazi waliompora fedha kabla ya
kumnyonga hadi kufa.
Yapo matukio mengi ya namna hiyo katika sehemu
mbalimbali nchini, lakini mengi kati ya hayo hayafanyiwi uchunguzi wa
kujua chanzo.
Daktari wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa na
Kiongozi wa Idara ya Uchunguzi wa Vifo katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili (MNH), Innocent Mosha anasema ni muhimu kufanya uchunguzi wa
sababu za kifo ili kujiondolea shaka au wasiwasi wa kipi kilisababisha
kifo hicho.
Dk. Mosha anaelezea maana ya uchunguzi wa kifo na
kusema kuwa ni kitendo cha madaktari kutafuta chanzo kilichosababisha
kifo cha mtu na kujiridhisha au ndugu kuridhika pasipo shaka.
“Watanzania walio wengi bado hawafahamu umuhimu wa
kufanya uchunguzi wa vifo vya ndugu zao, jambo ambalo linasababisha
wakati mwingine kupoteza ushahidi au kukosa cheti cha kifo ambacho kina
umuhimu mkubwa katika masuala ya mirathi,” anasema Dk Mosha
Anasema uchunguzi wa kifo si kwa ajili ya polisi
wa upelelezi tu, bali ni mchakato unaotakiwa kufanywa na ndugu wa
marehemu ili kujiridhisha na sababu ya kifo cha ndugu yao.
Anaongeza kuwa tatizo kubwa hapa nchini ni kuwa
watu wengi hawaelewi maana na umuhimu wa kuchunguza miili ya ndugu zao
ili kujua chanzo au sababu za vifo vyao.
Mchakato wa Uchunguzi
Kwanza, Dk. Mosha anasema uchunguzi wa kifo kwa
matukio yanayohusisha polisi, huhitaji taarifa ya utangulizi ambapo
polisi hutakiwa kutoa maelezo ya awali kuhusu marehemu.
Anasema pia kuwa katika matukio hayo, ndugu zaidi
ya mmoja huhitajika kwa ajili ya kumtambua marehemu, sanjari na
kujaza fomu ya maelezo mafupi. “Baada ya polisi kutoa maelezo yao ambayo
kwa kawaida huwa ni mafupi, daktari huendelea na uchunguzi wake
kulingana na ujuzi wake,” anasema.
chanzo mwananchi
chanzo mwananchi
No comments:
Post a Comment