Thursday, 13 March 2014

DARAJA LA KIGAMBONI

Pembezoni mwa Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Tanzania (Tec), ujenzi unaendelea wa barabara na daraja la kuunganisha Mji wa Kigamboni na Jiji la Dar es Salaam, eneo la Mkondo wa Kurasini. Ujenzi huo unafanywa na kampuni mbili kutoka nchini China.
Kampuni hizo ni; China Railway Jiangchang (T) Ltd na China Major Bridge, mradi ambao unatarajiwa kukamilika Januari 2015 ukigharimu dola 136 milioni za Marekani, fedha ambazo asilimia 60 zinatolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na kiwango kingine kinalipwa na serikali.
Ujenzi huo unafanyika ikiwa ni sehemu ya kuwaondolea kero ya Kivuko wakazi wapatao 679,291 sawa na asilimia 5.7 ya watu wote wa Dar es Salaam na idadi hiyo ni tofauti na mamia wengine ambao wanaenda eneo hilo kila siku kwa ajili ya shughuli tofauti zikiwamo za kiuchumi.
Eneo la Kigamboni ambalo limelengwa kuwa mji mpya wa kisasa, lina utajiri mkubwa wa mazao mbalimbali ya chakula, biashara kama vile mbogamboga, matunda, viazi vitamu, magimbi, nazi, korosho na mazao ya baharini wakiwamo samaki, mapambo ya majumbani na bidhaa nyingine.
Pia mji huo una hifadhi historia kwani maeneo ya Mbwamaji, Puna, Kimbiji, Pembamnazi, Buyuni na kwingineko kuna mabaki ya majengo ya kihistoria ambayo hata hivyo yanatoweka kutokana na utunzaji na harakati za ujenzi wa nyumba za kisasa.
Pia eneo hilo linasifika kwa kuwa na fukwe zenye mchanga wa kuvutia na mandhari nzuri za kupendeza hali ambayo inachangia kuwavutia watalii na wageni wengine wanaotembelea eneo hilo ambalo pia upande mwingine ina hazina kubwa ya jiwe la jasi ambalo hutumika kutengenezea saruji.
Kulingana na mkandarasi ambaye ni mbunifu wa mradi huo ambalo ni la kuning’inia (Cable-Stayed Bridge), lina urefu wa mita 680 na upana wa mita 27.5 na linatarajiwa kuwa mbadala wa Kivuko cha Kigamboni ambacho kina pantoni za Mv Kigamboni na Magogoni.
Ujenzi huo unakaribia kukamilika, lakini hadi sasa gharama za kulitumia daraja hilo kwa wananchi wa kawaida, wenye magari, baiskeli, mikokoteni na vyombo vingine bado hazijainishwa. Suala hilo linawaacha watu weni katika maswali mengi kuliko majibu.
Ingawa hakijatajwa kiwango kitakachokuwa kinatozwa kama ada na ushuru mwingine, lakini bado kuna utata iwapo mradi huo utakamilika kwa wakati kutokana na sababu nyingi ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa mradi umefikia zaidi ya asilimia 50 ya ujenzi wake, lakini kuna utata iwapo ujenzi utakamilika kwa wakati.
Hali hiyo inatokana na ukweli kuwa hadi hivi sasa serikali haijatoa kiasi chochote kati ya asilimia 40 ya fedha ambazo wanatakiwa kuchangia ili kukamilisha mradi huo hali ambayo inadaiwa kukwamisha upatikanaji wa fedha za fidia kwa baadhi ya watu ambao wanaguswa na mradi.
Msimamizi wa mradi huo, Mhandisi Karimu Mataka wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), anakiri serikali kutokutoa fedha ambazo iliahidi hadi sasa, na hali hiyo imechangia mradi kushindwa kukamilika Januari mwakani kama ilivyokadirwa na badala yake sasa unatarajiwa kukamilika Juni mwakani.
John Ngoma maarufu kwa jina la Jitu,mkazi wa eneo la Kijibweni ambaye eneo lake limechukuliwa kwa ajili ya kutoa nafasi ya utekelezaji wa mradi huo anasema ni vizuri wakaelezwa kiasi cha fidia watakachopewa kabla ya uthamini kufanywa jambo ambalo linapingwa na mfumo mzima wa fidia.
CHANZO MWWANANCHI

No comments:

Post a Comment