Thursday, 13 March 2014

ELIMU KWA WAJASILIAMALI

Katika hali ya kawaida mtu unapoamua kuwekeza au kufanya biashara ya aina yoyote, suala la kupata faida au hasara ni lazima liwe kichwani mwako. Jambo lingine ni la kuangalia ni kuhusu muda ambao utatumika ili uwekezaji wako uanze kuleta tija pamoja na muda unaotumia katika kusimamia biashara au uwekezaji wako.
Uwekezaji unapitia hatua mbalimbali kwani kuna kipindi inawezekena soko lipo katika hali nzuri au mbaya. Endapo ikatokea hali kuwa mbaya mwekezaji makini anapaswa awe na subira kwani wakati mwingine hicho ni kipindi cha mpito.
Kwa wale ambao suala la subira halipo, siku zote wanachukua uamuzi haraka kwa kuuza kitega uchumi husika na kupoteza fursa ya kupata faida zaidi. Ili uwe mwekezaji mzuri unapaswa uwe mvumilivu. Uvumilivu unategemea na kipato au umri kwa mfano, uvumilivu kati ya mtu ambaye ni kijana hutofautiana na mzee au mtu aliyepevuka ujana.
Uzoefu unaonyesha kwamba mwekezaji anayekaribia kustaafu, uwezo wa kuvumilia hasara huwa ni mdogo ukilinganisha na mwekezaji ambaye ni kijana. Mwekezaji wa mwanzo anakuwa anaangalia kile ambacho amekichuma kwa muda mrefu, hataki kukipoteza kwani uwezo wa kukirudisha unakuwa mdogo au haupo-tofauti na mwekezaji ambaye ni kijana kwani ana muda mrefu wa kuweza kufidia hasara ambayo anaweza kuipata kupitia uwekezaji ambao ameufanya uwe ni kupitia masoko ya mitaji au sehemu nyingine.
Kuna watu wengine wanasema uwekezaji kupitia masoko ya mitaji, upatikanaji wa faida ni mdogo sana ukilinganisha na aina nyingine ya biashara kwa mfano, ufugaji wa kuku, kufungua duka la vifaa vya ujenzi, biashara ya magari na aina nyingine ya biashara ambazo zinapatikana katika ulimwengu huu.
Katika makala haya nitatofautiana na watu wenye mawazo kama hayo hapo juu. Uwekezaji kupitia masoko ya mitaji una nafuu ingawa faida inayopatikana siyo kubwa sana, pia ikumbukwe kuwa siku zote uwekezaji wenye kutoa faida ya wastani ni endelevu.
Unafuu mwingine ambao ninauzungumzia ni katika suala zima la kupoteza mtaji wote, katika aina hii ya uwekezaji suala kama hilo linakuwa halipo kwani kuna kampuni ambazo hazifanyi vizuri sokoni, lakini wale ambao waliwekeza katika hizi kampuni hawajapoteza fedha zao zote.
Kitu kama hiki hakipo katika biashara nyingine kama vile ufugaji kuku, kwani katika aina hii ya biashara unaweza kuwa umeingia gharama kubwa za kukuza kuku hao, ghafla ugonjwa ukawakumba na wote wakafa, moja kwa moja utakuwa umepoteza mtaji wako wote. Wakati mwingine unakuta mtu amestaafu ndiyo anaanza kufanya biashara kwa kutumia fedha alizolipwa wakati wa kustaafu bila hata kufanya utafiti namna ya biashara ilivyo kisa ameona fulani anafanya na kusikia maneno kuwa biashara fulani inalipa sana na yeye anaingia kichwa kichwa.
Ili mtu afanikiwe anapaswa uwe na uzoefu na biashara unayotaka kufanya, katika ili wengi wao wanapokimbilia kununua magari ya abiria na baada ya muda wanajikuta hawezi kutengeneza faida ambayo walikuwa wanaitegemea awali, hapo ndiyo muda wa kufilisika na kuanza kuishi maisha magumu kwani hakuna mshahara ambao utakuwa unaingia zaidi ya kutegemea pesheni ambayo haiwezi kukidhi mahitaji yako yote.
Wale ambao wanakuwa wamewekeza kupitia masoko mitaji na kampuni walilizowekeza wanakuwa katika hali nzuri ya kifedha kwani wanakuwa na uhakika wa kupata au kuingiza fedha kwa kila baada ya muda fulani iwe ni kwa mwaka au kila baada ya miezi sita kupitia gawio.

No comments:

Post a Comment