Dar es Salaam. Rais Jakaya
Kikwete amesema Serikali imenuia kumaliza kabisa ujangili nchini, ikiwa
ni hatua ya kunusuru wanyama walio hatarini kutoweka katika hifadhi za
taifa.
Hakusita kusisitiza kwamba, nia ya dhati ya
Serikali ni kuhakikisha mkakati huo unakamilika, japokuwa kumekuwa na
changamoto zinazotokana na ukubwa wa hifadhi hizo na uhaba wa vitendea
kazi pamoja na askari wa wanyamapori.
Akizungumza wakati wa kupokea magari 11 ya kisasa
kwa ajili ya kusaidia operesheni ya kupambana na ujangili kutoka kwa
Shirika la Frankfurt Zoological Society (FZS) la Ujerumani, Kikwete
alisema tatizo hilo limekuwa la muda mrefu, lakini juhudi za kulikomesha
zinafanyika.
Alisema, pamoja na ukubwa wa tatizo hilo, bado
kuna tatizo la uhaba mkubwa wa wafanyakazi wanaotakiwa kudhibiti
majangili, ambapo kwa sasa kuna wafanyakazi 1,155 sawa na asilimia 24 tu
ya mahitaji halisi ya wafanyakazi 4,000 wanaohitajika.
“Mwaka uliopita, Serikali ilisimamia ajira ya wafanyakazi 449 na sasa kuna ajira ya wafanyakazi 500.
Kwa maana hiyo tutafikisha wafanyakazi wapya 949
na kufanya mahitaji ya wafanyakazi wapya kuwa 4,000 zaidi ili kuwezesha
utekelezaji wa majukumu kwa viwango vya kimataifa,” alisema.
Kwa mujibu wa viwango vilivyopo sasa, mfanyakazi
mmoja anasimamia eneo la kilometa za mraba 169 ikilinganishwa na viwango
vya kimataifa vya kilometa za mraba 25 kwa kila mfanyakazi mmoja.
Rais Kikwete alisema kwa sasa Serikali itaendelea
kuajiri idadi hiyo ya wafanyakazi kila mwaka kwa miaka mitatu ijayo ili
kuhakikisha pengo lililopo linazibwa.
Alisisitiza kuwa, kampeni dhidi ya ujangili ni
suala la kimataifa na Tanzania au nchi zilizoathirika hazitaweza
kulikabili bila ushirikiano wa kimataifa.
Alisema upo ulazima wa kuteketeza mitandao yote ya
ujangili na kuwawajibisha ipasavyo watakaonaswa, kwani kwa kufanya
hivyo kutasaidia kulinda urithi huo wa dunia.
Ukosefu wa vifaa
Akifafanua, Rais Kikwete alisema kuongeza idadi
hiyo ya wafanyakazi pekee haitakuwa na maana iwapo hawatakuwa na vifaa
maalumu vya kisasa vitakavyowawezesha kukabiliana ipasavyo na tishio la
ujangili.
CHANZO MW ANANCHI
CHANZO MW ANANCHI
No comments:
Post a Comment