Tuesday, 11 March 2014

JK :ATANGAZA VITA NA MAJANGILI




Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amesema Serikali imenuia kumaliza kabisa ujangili nchini, ikiwa ni hatua ya kunusuru wanyama walio hatarini kutoweka katika hifadhi za taifa.
Hakusita kusisitiza kwamba, nia ya dhati ya Serikali ni kuhakikisha mkakati huo unakamilika, japokuwa kumekuwa na changamoto zinazotokana na ukubwa wa hifadhi hizo na uhaba wa vitendea kazi pamoja na askari wa wanyamapori.
Akizungumza wakati wa kupokea magari 11 ya kisasa kwa ajili ya kusaidia operesheni ya kupambana na ujangili kutoka kwa Shirika la Frankfurt Zoological Society (FZS) la Ujerumani, Kikwete alisema tatizo hilo limekuwa la muda mrefu, lakini juhudi za kulikomesha zinafanyika.
Alisema, pamoja na ukubwa wa tatizo hilo, bado kuna tatizo la uhaba mkubwa wa wafanyakazi wanaotakiwa kudhibiti majangili, ambapo kwa sasa kuna wafanyakazi 1,155 sawa na asilimia 24 tu ya mahitaji halisi ya wafanyakazi 4,000 wanaohitajika.
“Mwaka uliopita, Serikali ilisimamia ajira ya wafanyakazi 449 na sasa kuna ajira ya wafanyakazi 500.
Kwa maana hiyo tutafikisha wafanyakazi wapya 949 na kufanya mahitaji ya wafanyakazi wapya kuwa 4,000 zaidi ili kuwezesha utekelezaji wa majukumu kwa viwango vya kimataifa,” alisema.
Kwa mujibu wa viwango vilivyopo sasa, mfanyakazi mmoja anasimamia eneo la kilometa za mraba 169 ikilinganishwa na viwango vya kimataifa vya kilometa za mraba 25 kwa kila mfanyakazi mmoja.
Rais Kikwete alisema kwa sasa Serikali itaendelea kuajiri idadi hiyo ya wafanyakazi kila mwaka kwa miaka mitatu ijayo ili kuhakikisha pengo lililopo linazibwa.
Alisisitiza kuwa, kampeni dhidi ya ujangili ni suala la kimataifa na Tanzania au nchi zilizoathirika hazitaweza kulikabili bila ushirikiano wa kimataifa.
Alisema upo ulazima wa kuteketeza mitandao yote ya ujangili na kuwawajibisha ipasavyo watakaonaswa, kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia kulinda urithi huo wa dunia.
Ukosefu wa vifaa
Akifafanua, Rais Kikwete alisema kuongeza idadi hiyo ya wafanyakazi pekee haitakuwa na maana iwapo hawatakuwa na vifaa maalumu vya kisasa vitakavyowawezesha kukabiliana ipasavyo na tishio la ujangili.
CHANZO MW ANANCHI

No comments:

Post a Comment