Thursday, 6 March 2014

HATUFUNGANI NI UWEKEZAJI BORA

Serikali inapotaka kufanya shughuli za maendeleo inaweza kuamua kuuza hatifungani (bond) kwa umma na wananchi watakaponunua hizo hatifungani wanakuwa wamewekeza. Hivyo utakuwa ni wajibu wa Serikali kuwalipa riba hawa wawekezaji katika hatifungani hizo.
Jiji au Halmashauri pia zinaweza kuuza hatifungani katika kuendesha shughuli za maendeleo katika jiji au halmashauri husika. Kwa mfano ujenzi wa madaraja, hospitali pamoja na ujenzi wa shule.
Kampuni binafsi pia inapotaka kufanya shughuli za maendeleo, inakopa fedha katika taasisi za fedha au kuuza hatifungani. Endapo kampuni imeamua kuuza hatifungani inakuwa inakwepa gharama za kukopa katika taasisi za fedha.
Hatifungani ni hati ya deni ambayo kampuni au serikali huwalipa wawekezaji kwa makubaliano maalumu na riba kulipwa na marejesho baada ya kuiva kwa hatifungani.
Mwekezaji ambaye amewekeza katika hatifungani anakuwa ni mwanahati. Hatifungani za Serikali na za kampuni binafsi zinauzwa na kununuliwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).
Kuna hatifungani za Kampuni binafsi mbalimbali ambazo zimeorodheshwa katika Soko la DSE. Kati ya kampuni hizo ni Tanzania Breweries Ltd, ALAF Ltd, Standard Chartered Bank Ltd, Promotion of Rural Initiatives and Development Enterprises Ltd (PRIDE) pamoja na Bank M. Kati ya kampuni hizo, ziko ambazo zinatoa riba mpaka asilimia 15.
Ili kampuni iweze kuuza hatifungani kwa umma inatakiwa ipate kibali kutoka kwa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana. Katika hili hakuna tofauti na pale kampuni inapotaka kuuza hisa kwa umma katika soko la awali.
Hapa utayarishaji wa waraka wa toleo unatakiwa uwe umeandaliwa pia. Waraka wa toleo unakuwa umebeba vitu vingi. Moja ya vitu hivyo ni jinsi gani fedha zitakazopatikana zitatumika, kiwango cha chini cha kufanya uwekezaji pamoja na athari za uwekezaji (risk factor) katika kampuni husika.
Mwekezaji mtarajiwa anapowekeza katika hatifungani, iwe za serikali au kampuni binafsi, anapata riba. Katika upande wa uwekezaji katika hatifungani za serikali, mwekezaji anakuwa na asilimia kubwa ya kupata riba ila kwa upande wa kampuni binafsi mwekezaji anatakiwa afanye uchunguzi kuhusu kampuni husika kwani asipofanya uchunguzi anaweza akawekeza sehemu ambayo si salama.
Mwekezaji katika hatifungani za kampuni binafsi anatakiwa ajue moja ya mambo kama mfumo wa mtaji wa kampuni, uongozi uliopo katika madaraka, kampuni husika ipo katika sekta gani ya biashara pamoja na usalama wa kulipwa riba.
Katika suala la usalama wa kulipwa riba, wakati nipo chuoni walimu walikuwa wanatuambia kuwa unapowekeza katika hatifungani za serikali ni vigumu kutopata riba au si rahisi kupoteza fedha kutokana na kuwekeza katika hizo hatifungani.
Katika hali ya sasa mambo yamebadilika kwani hata Serikali inaweza kuyumba kiuchumi. Mfano mzuri ni baada ya kutokea mdororo wa uchumi duniani kwani nchi mbalimbali zilikumbwa na huo janga hilo hata watu ambao walifanya uwekezaji waliathiriwa kwa kiwango kikubwa. :{chanzo mwananchi}

No comments:

Post a Comment