Thursday, 6 March 2014

BUNGE LA KATIBA LAPITISHA KANUNI KWA MBINDE


Mwenyekiti wa muda wa Bunge la katiba,Pandu kificho. 
Bunge Maalumu la Katiba limepitisha kanuni ya kuwazuia waandishi wa habari kuingia katika vikao vya kamati za chombo hicho, hatua ambayo inaelezwa ni kinyume na Katiba inayotoa uhuru wa wananchi kupata habari.
Kanuni hiyo ilipitishwa jana baada ya malumbano makali yaliyowagawa wajumbe wa bunge hilo, baadhi wakipinga kifungu hicho kwa sababu kinavunja Katiba ya nchi inayotoa uhuru kwa waandishi kukusanya na kusambaza habari na wengine wakiunga mkono kuwazuia.
Kanuni hiyo ilipitishwa kwa mbinde huku baadhi ya wajumbe wakiendelea kushikilia msimamo wa kuikataa, hata baada ya Mwenyekiti wa Muda wa bunge hilo, Pandu Ameir Kificho kuridhia kipite. Wajumbe waliopinga kanuni hiyo ni Joshua Nasari, Moses Machali, Peter Serukamba, Ezekiah Wenje na Maria Sarungi.
Baadhi ya wajumbe akiwamo Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga walisimama kutaka kuzungumza lakini hawakupata fursa hiyo.
Mjumbe aliyekuwa mwiba kwa Tasnia ya Habari ni, Dk Harrison Mwakyembe ambaye aliwashawishi wajumbe kufunga mjadala huo ili wasonge mbele kwa madai kuwa hata yeye pia ni mwanahabari. “Hakuna upande usiotambua umuhimu wa vyombo vya habari katika mchakato huu... Tunachotofautiana ni jinsi na namna
ya ushiriki wa vyombo vya habari,” alisema Dk Mwakyembe. Alisema Taifa limeingia katika kipindi maalumu kama cha vita na kwa msingi huo, kanuni zinabadilika kulingana na mazingira na kwamba vyombo vya habari vinapaswa kulitambua hilo.
Hata hivyo, Kifungu cha 57 (3) katika kanuni hiyo kilipita baada ya kufanyiwa marekebisho kuondoa maneno ‘mwenyekiti anaweza kutoa taarifa’ badala yake, ikawa ‘ni lazima kutoa taarifa.’
Kanuni hiyo inampa mamlaka mwenyekiti wa kamati au mjumbe yeyote kwa idhini yake, kutoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu mambo yaliyojitokeza kwenye kikao.
Mjadala wakwama
Mvutano juu ya kifungu hicho ulianza juzi jioni wakati baadhi ya wajumbe walipotofautiana.
Akiwasilisha maoni ya Kamati ya Kumshauri Mwenyekiti, Mjumbe George Simbachawene alisema iwapo waandishi wataruhusiwa wangeweza kutoa taarifa zisizochujwa ambazo zitawachanganya wananchi.
Hata hivyo, Mjumbe wa bunge hilo, Ezekiah Oluoch alisema kisheria kanuni hiyo ilikuwa inakwenda kinyume na Ibara ya 18 ya Katiba ya nchi ambayo kimsingi, ndiyo sheria mama. Aliisoma ibara hiyo akisema kama wajumbe wataruhusu kupitishwa kwa kifungu hicho, litakuwa kosa kubwa la kuvunja katiba ya nchi
.chanzo mwananchi

No comments:

Post a Comment