Monday, 22 September 2014

SIMBA KAKABWA KOO NA WAGOSI WA KAYA


0
Share

Dar es Salaam. Makosa ya mabeki wa Simba yaliyofanywa dakika za majeruhi, yaliipa sare ya kwanza msimu huu baada ya kufungana 2-2 na Coastal Union ya Tanga katika mechi ya kupendeza iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jana.Katika mchezo huo, Coastal walitumia dakika nane za majeruhi kipindi cha pili kufunga bao la kusawazisha na kuinyima Simba ushindi katika mechi yao ya kwanza msimu huu.Bao la Coastal lilitokana na makosa ya kiufundi ya mabeki wa Simba walioshindwa kuweka ukuta imara kuzuia kiki ya adhabu ndogo iliyopigwa na Ramadhan Salum dakika ya 82 na kwenda moja kwa moja kwenye kamba za Wekundu hao.
Kosa la kwanza lililoigharimu Simba na kuipa Coastal kupata bao la kwanza, lilifanywa na kiungo Pierre Kwizera aliyeshindwa kuumiliki vizuri mpira kabla ya kunaswa na wachezaji wa Coastal Union na Lutimba Yayo Kato kuutumbukiza wavuni kwa kiki ya karibu na lango.
Kwa matokeo ya mchezo wa jana, Simba na Coastal Union zimezoa pointi moja kila mmoja.
Mchezo wa jana uliokamilisha mechi za kwanza za raundi ya kwanza ya ligi hiyo, ulianza kwa Simba kusalimia lango la wapinzani wao na kuandika bao la kwanza kupitia kwa Shaaban Kisiga. Kisiga alifunga bao hilo kwa mpira wa faulo dakika ya saba kabla ya Amis Tambwe kufumania nyavu dakika ya 36 akiunganisha kwa kichwa akimalizia krosi ya Emmanuel Okwi.
Kwa upande mwingine, juhudi za Simba kupata mabao, zilichangiwa kwa kiasi kikubwa na Okwi kwani bao la kwanza, aliangushwa nje ya 18 na beki wa Coastal, Tumba Swedi kabla ya Kisiga kufunga kwa faulo, pia alipiga krosi ambayo iliunganishwa na Tambwe kuandikia bao la pili.Jitihada za Union kusaka bao zilizaa matunda katika dakika ya 67 baada ya Lutimba Yayo Kato kufanikiwa kumtungua kipa wa Simba, Ivo Mapunda kufuatia pande la Itubu.
Ikishambulia mfululizo, Coastal Union ilisawazisha dakika ya 82 kupitia kwa Ramadhan Salum aliyetandika mpira wa faulo uliokwenda moja kwa moja nyavuni.
Simba waliianza mechi ya jana kwa kasi huku wakitawala sehemu ya kiungo, lakini mipira yao ya mwisho haikuwa makini na hivyo kushindwa kutengeneza nafasi za mabao huku Haruna Chanongo akipoteza chache walizozipata.
Katika kipindi cha kwanza, Coastal walitumia muda mwingi kulinda lango zaidi kuliko kushambulia, huku pia ikifanya mashabulizi ya kushtukiza wakimtumia mshambuliaji Itubu Imbem.
Kipindi cha pili, Simba walifanya mabadiliko kwa kuwatoa Chanongo na Tambwe na nafasi zao kuchukuliwa na Uhuru Selemani na Rafael Kiongera, wakati Coastal waliwatoa Seleman Kibuta, Razak Khalfan na Joseph Mahindi na nafasi zao kuchukuliwa na Lutimba Yayo Kato, Ayoub Yahaya na Abbas Athuman.
Mabadiliko hayo yaliwanufaisha Coastal kwani walipata mabao mawili. Akizungumza baada ya mechi kumalizika kocha wa Simba, Patrick Phiri alisema: “Coastal walicheza vizuri, sijafurahia matokeo tuliyoyapata ila tutajiandaa kwa ajili ya mechi ijayo.”

No comments:

Post a Comment